info@ttcl.co.tz
+255 22 210 0100

TTCL YAPELEKA HUDUMA ZAKE NANE NANE DODOMA

Shirika la Mawasiliano Tanzania –TTCL Corporation limepeleka huduma na bidhaa zake katika Maonesho ya Wakulima na Wafugaji maarufu Nane Nane yaliyofanyika Kitaifa katika Viwanja vya Nzuguni jijini Dodoma ili kukutana na wateja .

Shirika hilo lilitumia uwepo wa maonesho hayo kujitangaza na Kuongeza Ufahamu wa Huduma kwani Maonesho ya Nanenane yanakusanya watu kutoka sekta mbalimbali, ikiwemo wakulima, wafugaji, wajasiriamali, Mashirika ya Umma na binafsi na Wananchi kwa ujumla 

Shirika lilitoa elimu kuhusu huduma na bidhaa ikiwa ni pamoja na faida za matumizi ya intaneti yanavyoweza kuleta mapinduzi ya kiteknolojia katika sekta ya kilimo nchini.

Kwa kuwa Nanenane ni maonesho ya kilimo na ufugaji, TTCL ilionesha jinsi huduma za mawasiliano na teknolojia zinavyoweza kusaidia kuboresha shughuli za kilimo na ufugaji, kama vile umuhimu wa matumizi ya mawasiliano katika shughuli za kilimo na ufugaji na jinsi teknolojia hiyo inavyomwezesha mkulima na mfugaji kupata taarifa mbalimbali kuhusu masoko ya mazao yao na hivyo kujiendeleza kiuchumi na kuchangia katika maendeleo ya sekta ya kilimo na ufugaji hapa nchini.

Aidha kupitia mawasiliano, wakulima na wafugaji wanaweza kupata taarifa za hali ya hewa kwa wakati na kupanga shughuli zao kwa kufuaata ushauri wa wataalam ipasavyo, hivyo kupunguza athari za majanga ya asili.

TTCL ni mdau muhimu wa sekta ya kilimo na ufugaji Teknolojia ya mawasiliano inawawezesha wakulima na wafugaji kupata elimu mbalimbali kuhusu mbinu bora za kilimo na ufugaji kupitia Video, makala, na mafunzo ya mtandaoni.  

Uimara wa Mawasiliano nchini ni fursa muhimu inayowawezesha wakulima na wafugaji kuwasiliana moja kwa moja na wanunuzi wa bidhaa zao, hivyo kupunguza ulaghai na gharama za madalali hivyo kuongeza faida katika mapato yao.

Katika hatua nyingine TTCL iliyatumia maonesho hayo kuonesha jinsi shirika hilo linavyotoa huduma ya fedha mtandao kupitia Kampuni Tanzu ya T-PESA ambapo kupitia huduma hii wakulima na wafugaji wanao uwezo wa kuweka fedha zao katika simu zao na kupitia simu hizo wanaweza kufanya malipo na kutuma pesa zao kwenye akaunti zao za kibenki hali ambayo inafanya fedha zao kuwa salama Zaidi.

Mawasiliano ni nyenzo muhimu katika ulinzi na usalama wa mifugo kwani kwakutumia Teknolojia za mawasiliano kama GPS zinawezesha kufuatilia na kudhibiti mifugo, hivyo kupunguza upotevu na kuimarisha usalama wa mifugo.

Nane Nane ni sikukuu ya wakulima na Wafugaji hapa nchini ambayo huwapa fursa wakulima, Wafugaji Taasisi, Mashirika na wadau mbalimbali wa kilimo kote nchini kuonesha bidhaa zao na mafanikio yao katika mwaka husika.

Mwanzo, sikukuu hii ya Nane Nane iliitwa ‘Saba Saba’ ambapo ilikuwa ikiadhimishwa kila tarehe 7 ya mwezi Julai. Baadaye ilihamishiwa Agosti, 8 ya kila mwaka baada ya Saba Saba kufahamika zaidi kwa maonyesho ya wafanyabiashara.

Siku Kuu ya maonyesho ya wakulima iliadhimishwa kwa mara ya kwanza mwaka 1977 ili kuongezea nguvu sera ya Serikali ya wakati huo ya ‘Siasa ni Kilimo ‘, ambapo wakulima katika wilaya, Mkoa na kitaifa walionesha mazao yao halisi ya kilimo, wakaonyesha pembejeo za kisasa za killimo pamoja na kufundishwa namna ya kutumia pembejeo hizo kwa ustawi wa kilimo na Taifa.