info@ttcl.co.tz
+255 22 210 0100

RAIS SAMIA APONGEZA TTCL USHIRIKI TAMASHA LA KIZIMKAZI 2024

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amekabidhi cheti cha pongezi kwa Shirika la Mawasiliano Tanzania -TTCL kutokana na ushiriki wake wa kipekee katika Tamasha la Kizimkazi lililofanyika Kusini Unguja, Zanzibar.

Pongezi hizo ni kutambua mchango wa TTCL katika kuunga mkono shughuli za tamasha hilo ikiwa ni pamoja na michezo na shughuli mbalimbali za kijamii, kiutamaduni na kiuchumi wakati wa tamasha hilo.

Cheti hicho cha pongezi ni ishara ya kutambua umuhimu wa TTCL katika kuimarisha maendeleo ya jamii kidigitali na kufanikisha malengo ya kijamii, kiutamaduni na kiuchumi nchini.

TTCL ni miongoni mwa Wadau mbalimbali kama vile Mashirika ya Umma na binafsi, Taasisi na Wanachi mbalimbali walioshiriki Tamasha la Kizimkazi lililomalizika hivi karibuni wakiwa na lengo moja la kuunga mkono maendeleo ya kijamii, kiutamaduni na kiuchumi katika eneo la Kizimkazi Zanzibar.

Katika Tamasha hili la mwaka 2024, TTCL imeonesha ushiriki wake mkubwa kwa kudhamini tukio hili muhimu ili kuhakikisha lengo la kuunganisha watu, kutangaza vivutio vya utalii na biashara katika eneo la Kizimkazi na Tanzania kwa ujumla linafanikiwa. 

TTCL, kama mdhamini na mshirika muhimu katika tamasha hili lilipewa jukumu la kuhakikisha shughuli ya uzinduzi wa Pango la Paje, Fainali ya Mchezo wa Mpira wa Miguu na Usiku wa Bongo Fleva na Zenji Freva majukumu ambayo yalifanikiwa kwa kiwango kikubwa na kulifanya tamasha hilo kufikia malengo yake kwa mwaka huu wa 2024

Kimsingi ushiriki wa TTCL katika Tamasha la Kizimkazi 2024 umeongeza thamani ya tukio hilo kwa kuleta huduma zinazochochea maendeleo na kuimarisha mawasiliano, hivyo kufanikisha lengo la kuunganisha watu, utamaduni, na biashara katika eneo la Kizimkazi na Tanzania kwa ujumla.

Tamasha la Kizimkazi ni tukio ambalo limekuwa likiwakutanisha watu kutoka maeneo mbalimbali, wakiwemo wakazi wa Zanzibar, wageni kutoka Tanzania Bara, na hata kutoka nje ya nchi ambao hufika Kizimkazi kujionea urithi wa kipekee wa utamaduni wa Kizanzibari, kuhamasisha utalii, na kuimarisha mshikamano wa kijamii.