info@ttcl.co.tz
+255 22 210 0100

JAJI MKUU WA TANZANIA AVUTIWA NA HUDUMA YA CALL CENTER SABASABA

Jaji Mkuu waTanzania, Profesa Ibrahim Hamis Juma ametembelea banda la Shirika la Mawasiliano Tanzania TTCL wakati wa Maonesho ya 48 ya Kimataifa ya Biashara yanayofanyika katika Viwanja vya Mwalimu Nyerere Jijini Dar es Salaam.

Akiwa katika banda hilo Jaji Mkuu alipokelewa na Maafisa wa shirika hilo na kumuonesha maeneo mbalimbali ambayo yanasimamiwa na kutekelezwa na shirika hilo.

Aidha Maafisa hao walitoa maelezo ya jinsi TTCL inavyotekeleza majukumu yake ya kuhakikisha huduma za mawasiliano na huduma ya intaneti zinapatikana kwa Wananchi katika ubora na gharama nafuu.

Moja ya huduma iliyomvutia ni pamoja na huduma ya Kituo cha Huduma kwa Wateja (Call Center) na kutoa maagizo kwa watendaji wake kuhakikisha mfumo huo wezeshi wa huduma kwa wateja unafungwa katika Mahakama nchini ili kuboresha huduma za kimahakama na hivyo kuleta tija katika kuwahudumia wananchi.

Uwepo wa kituo cha call center katika Mahakama ni chachu ya kuboresha huduma kwani Wananchi wataweza kupiga simu moja kwa moja kwenye kituo cha call center ili kupata habari au msaada wowote unaohusiana na masuala mbalimbali yakiwemo ya mahakama.

Aidha mfumo huu unasaidia kupokea Malalamiko na Kutoa Msaada kuhusu huduma za mahakama na kutoa msaada wa awali au kuelekeza kesi hizo kwa hatua zinazostahili.

Katika hatua nyingi huduma hii itaisaidia Mahakama kutoa elimu kwa umma kuhusu taratibu za mahakama, haki za kisheria, na miongozo ya jinsi ya kufuata sheria. Na vilevile kupokea maoni kutoka kwa wananchi na kuboresha huduma zao kulingana na mrejesho huo.

Hivyo, kituo cha call center kinaweza kuwa chombo muhimu cha kuboresha upatikanaji na ufanisi wa huduma za Mahakama kwa umma. 

Call center ni kituo cha huduma kwa wateja kwa njia ya simu, kitakacho kuwezesha kuwasiliana na wateja wake kwa ukaribu zaidi kwa kupata taarifa mbalimbali za huduma zinazotolewa.